Pages

>>HATA MKTISHIA MAISHA WATU LAKINI UKWELI UTASEMWA,>>UJANGILI TZ


Gazeti la The Mail on Sunday la Uingereza limemwaga upupu baada ya kuchambua jinsi biashara ya meno ya tembo na pembe za faru ilivyokithiri nchini.

The Mail on Sunday ambalo ni gazeti dada la The Daily Mail, lilikuwa likitoa utangulizi wa habari kuhusu mkutano ulioitishwa na mwana wa mfalme wa Uingereza, Prince Charles, kujadili viumbe walio hatarini kutoweka, wakiwamo tembo na faru.

Katika mkutano huo Rais Jakaya Kikwete ni miongozi mwa viongozi wa nchi 50 walioalikwa. Hivyo gazeti hilo lilikuwa likiangalia kasi ya mauaji ya tembo nchini huku likidai kuwa Rais Kikwete amefumba macho.


Lakini kabla Uingereza pia taarifa hiyo haijakauka, televisheni ya ITV ya Uingereza imefanya uchunguzi wa biashara hiyo hapa Tanzania, na kuionyesha jinsi inavyofanyika.

Taarifa hiyo imekuwa shubiri kwa Serikali. Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu, amelaani vikali gazeti hilo huku Ikulu ikisema ni ya kipuuzi.

Kuna taarifa kuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali anajipanga kulishtaki gazeti hilo. Nisingependa kuingilia kesi hiyo inayoandaliwa, lakini nadhani bado kuna chembechembe za ukweli wa habari ile.

Tena ukweli unatokana na Serikali hiyo hiyo inayoruka kimanga. Tatizo tu ni kwamba ukweli siku zote unauma.

Mtu akishaambiwa ukweli, basi hutafuta njia za kujikosha ili aonekane mwema mbele za watu.

Hakuna ubishi kwamba kumekuwa na kasi kubwa ya mauaji ya tembo, nchini kiasi kwamba Serikali yenyewe iliamua kuanzisha Operesheni Tokomeza ambayo hata hivyo ilisitishwa.

Kwa mfano katika pori la akiba la Selous peke yake, tangu mwaka 1976 tembo wamepungua kutoka 110,000 kubakia 13,000. Ina maana kwamba tembo 100,000 wameshauawa.

Kwa mujibu wa mhifadhi mkuu wa pori hilo, Benson Kibonde, mwaka 1989 tembo walipungua na kufikia 30,000. Ndipo juhudi za kuhifadhi ikiwemo operesheni ya uhai, zilirejesha matumaini ambapo mwaka 1996 walifikia 70,000.

Lakini tatizo hilo limezidi hivi karibuni ambapo mwaka 2009, ndiyo kilikuwa kilele cha mauaji hadi idadi ya tembo imefikia 13.5 waliopo hadi sasa. Hii ni taarifa ya Serikali.