Pages

SHEKHE PONDA NI JAMBAZI?AMA AMEFANYA KOSA GANI KUBWA LA KUMFANYA YEYE AWE CHINI YA ULINZI MKALI HATA GEREZANI?






ULINZI anaopatiwa Kiongozi wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Tanzania, Sheikh Issa Ponda, akiwa mahabusu ndani ya Gereza la Segerea, Dar es Salaam, ni mkali na umeelezwa kuwa ni mara mbili ya ule aliokuwa akipatiwa awali wakati alipokuwa hapo, MTANZANIA Jumapili limedokezwa. Chanzo cha habari cha gazeti hili kilicho ndani ya gereza hilo, kilieleza kuwa ulinzi wa Sheikh Ponda umeimarishwa mara mbili zaidi kutokana na sababu za kiusalama.
Ulinzi ulioongezwa ni pamoja na ule wa maaskari magereza wanaomlinda, lakini pia vimeongezwa vikwazo ili kuwazuia watu kumuona ovyo.

Ni katika hali hiyo ya kuimarisha ulinzi dhidi ya kiongozi huyo, gazeti hili limedokezwa kuwa, hivi sasa Sheikh Ponda anaelezwa kulala katika chumba maalumu peke yake.

Akiwa mahabusu katika gereza hilo, mwaka jana kabla hajahukumiwa kifungo cha nje cha mwaka mmoja, Sheikh Ponda inadaiwa alikuwa akilala katika chumba maalumu, lakini wakiwa wawili yeye pamoja na Mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama wa Chadema, Wilfred Lwakatare.

Lwakatare kwa sasa yuko nje kwa dhamana, kutokana na kesi inayomkabili ya kula njama ya kutaka kudhuru kwa sumu.

Habari zilizolifikia gazeti hili, zinaeleza kuwa katika kuhakikisha usalama wa Sheikh huyo, hairuhusiwi mtu yeyote kumwona pasipo ruhusa kutoka ndani ya familia pamoja na kibali kutoka katika uongozi wa Magereza.

“Kwanza kwa sasa analala ‘special room’ (chumba maalumu), yaani fresh kabisa na ukitaka kumwona mpaka uidhinishwe na familia kutokana na ulinzi ulivyoimarishwa, chakula chake anachokula analetewa na ndugu zake pamoja na mke wake, cha hapa labda siku akipenda,” kilisema chanzo hicho.

Ni kwa namna hiyo ya kuimarisha ulinzi kwa Sheikh Ponda, takribani zaidi ya wiki mbili zilizopita serikali ilijikuta ikitoboka mfuko kwa kutumia kiasi cha Sh milioni 10,682,031 kama gharama za usafiri wa helikopta za kumpeleka na kumrudisha mahakamani mkoani Morogoro, katika kesi ya uchochezi inayomkabili.

Sheikh Ponda, ambaye anaelezwa kuigharimu serikali kiasi chote hicho cha fedha, ukiachana na gharama nyingine,

alikamatwa hivi karibuni na kurudishwa Segerea kwa mara ya pili akiwa bado anatumikia kifungo cha nje cha mwaka mmoja kwa kosa la uchochezi.

Ingawa taarifa rasmi hazijathibitishwa, Ponda anadaiwa kupigwa risasi akiwa katika harakati za kuondoka katika Mkutano aliofanya Morogoro, ambapo mpaka sasa anauguza jeraha katika mkono wake wa kulia.

Hata hivyo, kesi yake hiyo ya kwanza ilifutwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu na kufunguliwa nyingine mkoani Morogoro, anakotuhumiwa kuwa Agosti 10, mwaka huu, katika eneo la Uwanja wa Ndege, aliwaambia Waislamu wasikubali uundwaji wa kamati za ulinzi na usalama za misikiti, kwa madai kuwa zimeundwa na BAKWATA, ambao ni vibaraka wa CCM na serikali.

Pia anadaiwa kuwaagiza waumini hao kuwa endapo watu hao watajitokeza kwao na kujitambulisha kwamba ni kamati za ulinzi na usalama za misikiti, wafunge milango na madirisha wawapige.

Ilielezwa kuwa kauli hiyo ni kinyume cha agizo la Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, iliyotolewa na Hakimu V. Nongwa Mei 9, mwaka huu, ambayo ilimtaka Ponda ndani ya mwaka mzima kuhubiri amani.

Katika shitaka la pili, anadaiwa siku hiyo hiyo katika eneo la Uwanja wa Ndege, Morogoro, Ponda aliwaambia Waislamu kuwa serikali ilipeleka jeshi Mtwara kushughulikia suala la vurugu iliyotokana na gesi ili kuwaua, kuwabaka na kuwatesa wananchi, kwa sababu asilimia 90 ya wakazi hao ni Waislamu.

Kwamba, serikali haikufanya hivyo kwa wananchi wa Loliondo walipokataa Mwarabu asipatiwe kipande cha ardhi ya uwindaji baada ya kudai ni mali yao, kwa sababu asilimia 90 ya wakazi wa huko ni Wakristo.

Katika shitaka la tatu anadaiwa kuumiza imani za watu wengine kinyume cha kifungu cha sheria namba 390 na kanuni ya adhabu namba 35 cha mwaka 2002.

Hata hivyo, Sheikh Ponda ameyakana mashtaka hayo na kukubali baadhi ya vipengele.

0 comments:

Post a Comment